MAOFISA UGANI WATAKIWA KUWA NA SHAMBA LA MFANO LA ALIZETI KWA AJILI YA KUFUNDISHIA WAKULIMA

 


SERIKALI imewaagiza Maafisa Ugani wa Kata na Kijiji kuwa na shamba la mfano la alizeti ili kuwafundisha kwa vitendo wakulima na kuongeza uzalishaji wa zao hilo nchini.

Kauli hiyo imetolewa na Waziri wa Kilimo, Prof Adolf Mkenda Wilayani Mpwapwa Mkoani Dodoma wakati akifungua mkutano wa maafisa ugani kuhusu kanuni bora za alizeti kwa maafisa hao kutoka Mikoa ya Singida, Dodoma na Manyara.

Prof Mkenda amesema kama nchi ina changamoto mbili ambapo moja ni kuzalisha sana mafuta na nyingine ni kutafuta wanunuzi ili kuweza kufanikisha kudhibiti suala zima la uhaba wa mafuta.

Kutokana na hilo amesema maafisa Ugani wanakazi kubwa ya kuhakikisha wanatoa elimu ya uzalishaji zao la alizeti kwa vitendo kupitia mashamba darasa ambayo wanatakiwa kuwa nayo.

"Tuna changamoto ya uzalishaji, hatuzalishi vya kutosha ingawa uwezo wa kuzalisha tunao,hivyo kila afisa Ugani anapaswa kuwa na shamba darasa ili afundishe wakulima kwa vitendo katika eneo analofanyia kazi ili waweze kuzalisha kwa kiasi kikubwa,”Amesema Prof Mkenda.

Waziri Mkenda amesema lengo ni kuona Serikali inaepuka kutumia fedha nyingi kwa ajili ya kuagiza mafuta ya kula nje ya nchi badala yake yapatikane kwa wazalishaji wa hapa nchini.

"Ni lazima tutatue kitendawili hiki kuanzia zao moja hadi lingine ikiwemo kutoa elimu na kuwapa pembejeo wakulima ili kufanikisha kuondokana na uzalishaji mdogo,” Amesema Prof Mkenda.

Nae Mwenyekiti wa Halmashauri ya Mpwapwa, George Fuime amebainisha kuwa haiwezekani kama nchi kulima zao la Alizeti kwa wingi lakini upatikanaji wa mafuta unakua mdogo hivyo amewataka maafisa ugani kuhakikisha wanatoa mafunzo hayo kwa vitendo kwa wakulima.

Fuime amesema ni vema wakatumia nafasi yao kutoa elimu ili wakulima wajue nini wanatakiwa kufanya ili waweze kuzalisha kwa tija.

CHANZO: MICHUZI TV


Comments

Popular posts from this blog